Ijumaa , 18th Aug , 2017

Mchezaji wa kutoka timu ya TMT, Rafael Msofe amesema pamoja na ushindi walioupata 'game 2' ya fainali za Sprite BBall Kings dhidi ya Mchenga BBall Stars bado wanakibarua kizito cha kuibadilisha timu yao ili waweze kushinda katika mechi ya kesho

Wachezaji wa TMT na Mchenga BBall Stars (jezi nyeupe) wakiwa katika mpambano.

Msofe amebainisha hayo baada ya kuisaidia timu yake kuweza kutoka kifua mbele kwa pointi 87-78 mchezo wa pili wa fainali hizo jambo ambalo wengi wao hawakutegemea kama ingekuwa hivyo.

"Bado kuna vitu viwili vitatu vya kuviweka sawa katika kikosi chetu ili katika mchezo wa kesho na mwingine wa nne tuweze kushinda pia. Sidhani kama kuna umuhimu wa kuenda mpaka game 5 maana watu wana vitu vingi vya kufanya", alisema Msofe.

Mchezaji wa TMT, Rafael Msofe.

Pamoja na hayo, Msofe amedai kuwa wanataka 'game 4' wamalize kila kitu ili waweze kuondoka na kile kitita cha Milioni 10 za mshindi wa kwanza.

Timu hizo mbili zitakutana tena Jumamosi ya kesho Agosti 19 katika viwanja vya Don Bosco Oysterbay Jijini Dar es Salaam ili waweze kucheza 'game 3' ambayo mshindi atakayepatikana katika mchezo huo atakuwa amejiweka katika nafasi nzuri ya ushindi endapo atashinda pia mchezo wa nne wa fainali hizo.