Jumapili , 13th Aug , 2017

Afisa habari wa klabu ya Simba, Haji Manara amempongeza Rais mpya wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia huku akipiga dongo kwa kudai enzi za kubebana zimeisha na sasa ni wakati wa kupeleka soka mbele.

Afisa habari wa klabu ya Simba, Haji Manara.

Manara amefunguka hayo kupitia ukurasa wake wa Istragram masaa machache kupita tokea Mwenyekiti wa Kamati ya uchaguzi mkuu wa (TFF), Revocatus Kuuli kumtangaza Wallace Karia kushinda nafasi hiyo kwa kura 95 kati ya 128 za wajumbe waliopiga kura kwenye uchaguzi huo, ambapo ataongoza kwa kipindi cha miaka minne kwa mujibu wa Katiba ya shirikisho hilo.

"Enzi za kubebana zimeisha TFF,na Simba hatutaki mbeleko tunataka haki, narudia haki. Hongera Wallace karia na Michael Wambura pelekeni soka mbele", ameandika Manara. 

Kwa upande mwingine, timu ya Simba leo inatarajiwa kushuka dimbani kukipiga na Kagera Sugar katika mechi yao ya kirafiki itakayofanyika katika uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam.