Jumatano , 14th Jun , 2017

Kocha Mkuu wa timu ya Tanzania 'Taifa Stars', Salum Mayanga ametangaza majina ya wachezaji 22 watakaounda kikosi kinachokwenda kushindana kuwania Kombe la Cosafa nchini Afrika Kusini inayotarajiwa kuanza Juni 25 mwaka huu.

Michuano hiyo, inayoandaliwa na Baraza la Mpira wa Miguu la nchi za Kusini mwa Afrika ambako Tanzania ni mwanachama wa Cecafa, imepata mwaliko kushiriki michuano hiyo.

Tanzania imepangwa kundi A ambako wapinzani wake ni Mauritius, Malawi na Angola wakati Kundi B ni Msumbiji, Shelisheli, Madagascar na Zimbabwe. Timu za Botswana, Zambia na Afrika Kusini kadhalika Namibia, Lesotho na Swaziland zitakuwa na mechi maalumu (play off) ili kuingia robo fainali.

KIKOSI KAMILI

Kwa mujibu wa Mayanga, kikosi hicho kinaundwa na makipa Aishi Salum Manula  (Azam FC), Benno David Kakolanya  (Young Africans SC) na Said Mohammed Said (Mtibwa Sugar FC).

Walinzi wa pembeni upande wa kulia ni Shomari Salum Kapombe (Azam FC) na Hassan Hamis Ramadhan 'Kessy' (Young Africans SC) wakati upande wa kushoto wapo Gadiel Michael (Azam FC) na Amim Abdulkarim (Toto Africans FC).

Walinzi wa kati ni Erasto Nyoni  (Azam FC), Salim Hassan Abdallah (Mtibwa Sugar), Abdi Banda (Simba SC) na Nurdin Chona (Tanzania Prisons) wakati viungo wa kuzuia kuwa ni Himid Mao (Azam FC) na Salmin Hoza wa Mbao FC.

Kadhalika wako viungo wa kushambulia ambao ni Mzamiru Yassin Selembe (Simba), Simon Happygod Msuva (Young Africans SC), Raphael Daudi (Mbeya City) na Shizza Ramadhani Kichuya (Simba SC).

Katika safu ya ushambuliaji wamo Thomas Emmanuel Ulimwengu (AFC Eskilstuna – Sweden), Mbaraka Abeid Yusufu (Kagera Sugar), Stamili Mbonde, Elius Maguli (Dhofar SC) na Shabani Idd Chilunda (Azam FC).