Ijumaa , 13th Oct , 2017

Katika mwendelezo wa ligi kuu ya soka Tanzania Bara VPL, leo umepigwa mchezo mmoja wa raundi ya 6 kwenye uwanja wa CCM Kirumba kati ya wenyeji Mbao FC dhidi ya Mbeya City.

Mbao FC ikiwa nyumbani imelazimishwa sare ya mabao 2-2 kwenye mechi ambayo ilikuwa na upinzani wa hali ya juu.

Mbao FC ndio walianza kugusa nyavu za Mbeya City mapema dakika ya tatu kupitia kwa Yusuf Ndikumana kabla ya kuongeza bao la pili kupitia kwa Ndaki ambapo hadi timu hizo zinakwenda mapumziko Mbao FC ilikuwa mbele kwa mabao 2-0.

Kipindi cha pili Mbeya City walirejea uwanjani kwa kasi ambapo dakika ya 55 walifunga bao la kwanza kupitia kwa Eliud Ambokile. Bao hilo liliwarejesha mchezoni na kuongeza mashambulizi hadi walipofanikiwa kusawazisha bao la pili kupitia kwa Ramadhani dakika ya 64.

Mbeya City imefikisha alama 8 baada ya michezo 6 ikiwa katika nafasi ya 7. Mbao FC imefikisha alama 6 baada ya michezo 6 ikishika nafasi ya 9. Ligi hiyo itaendelea kesho kwa jumla ya michezo 6 kupigwa kwenye viwanja mbalimbali.