Jumamosi , 25th Aug , 2018

Timu ya Kikapu ya Mchenga Bball Stars imefanikiwa kuweka historia ya kutetea ubingwa wake wa Sprite Bball Kings, kwa kuifunga Flying Dribbllers kwa pointi 87 dhidi ya 76 kwenye mchezo wa game 3 ya 'best of five' za fainali uliomalizika usiku huu kwenye uwanja wa ndani wa taifa.

Wachezaji wa Mchenga Bball Stars wakiwa na zawadi zao baada ya kukabidhiwa.

Mchenga wamechukua ubingwa huo kwa kushinda game zote tatu mfululizo yaani (Swipe) kati ya tano za fainali hivyo kuwanyima furaha wapinzani wao Flying Dribbllers kwa mara ya pili mfululizo baada ya kuwafunga kwa aina hii hii kwenye nusu fainali ya michuano hiyo mwaka 2017.

Katika game 1 Mchenga walishinda kwa pointi 103 dhidi ya 73 za Flying Dribblers, kabla ya kushinda kwa pointi 85 kwa 65 kwenye game 2 na leo kumalizia kazi kwa ushindi wa pointi 87 kwa 76.

Katika ushindi huo wa Mchenga Bball Stars mchezaji Baraka Sadick amekuwa na msaada mkubwa hali ambayo imepelekea kuibuka kama 'Most Valuable Player' wa mashindano kwa mwaka 2018.

Baraka amefunga pointi 239 katika michezo 8 aliyocheza. Katika michezo hiyo amekuwa na wastani wa kufunga pointi 30 katika kila mchezo. Katika mchezo wa leo Baraka amefunga pointi 33 kati ya 87 za timu yake.

Timu zote zimekabidhiwa zawadi ambazo ni shilingi milioni 3 kwa mshindi wa pili Flying Dribbllers, milioni mbili na tuzo kwa 'MVP' ambaye ni Baraka Sadick na milioni 10 kwa mabingwa ambao ni Mchenga Bball Stars. Sprite Bball Kings inaandaliwa na East Afarica Television chini ya udhamini wa kinywaji baridi cha Sprite.