Jumamosi , 28th Nov , 2020

Michuano ya timu za taifa za vijana chini ya umri wa miaka 20 ukanda wa Afrika Mashariki na kati 'CEACFA U20' imefikia hatua ya nusu fainali huku timu za Ngorongoro Heroes ya Tanzania ambao ndiyo wenyeji, Kenya, Uganda na Sudan ya Kusini zikitaraji kuchuana siku ya Jumatatu Novemba 30.

Kikosi cha Ngorongoro Heroes kikiwa mazoezini

Mchezo wa nusu fainali ya kwanza Timu ya Taifa ya Vijana ya Uganda watashuka dimbani kukipiga dhidi ya Timu ya Taifa ya Vijana ya Kenya majira ya saa sita kamili mchana kwenye uwanja wa Black Rhino Academy uliopo Karatu mkoani Arusha.

Bingwa wa mchezo huo atakutana fainalii kucheza na bingwa wa mchezo wa nusu fainali ya pili ambapo wenyeji Tanzania 'Ngorongoro Heroes' wanatazamiwa kukupiga na timu ya taifa ya vijana na Sudan Kusini saa tisa na nusu alasiri pia kwenye uwanja wa Black Rhino Academy karatu jijini Arusha.

Fainali ya michuano hiyo iliyoanza tarehe 22 mwezi huu inataraji kuchezwa tarehe 2 mwezi disemba jijini Arusha huku wenyeji wa michuani hiyo timu ya vijana ya Tanzania 'Ngorongoro Heroes' inayonolewa na Jamhuri Kihwelo 'Julio' ikipewa nafasi kubwa ya kubeba kombe hilo.