Jumanne , 18th Apr , 2017

Kamati ya Katiba, Sheria na Hadhi za Wachezaji ya TFF imeshindwa kuamua suala la Simba na Kagera Sugar kuhusu point 3 za kagera ilizopewa Simba, baada ya malalamiko ya malalamiko kuwa Kagera walimchezesha mchezaji kinyume na kanuni.

Celestine Mwesigwa, Katibu Mkuu TFF

Kamati hiyo ambayo imekaa leo, imeshindwa kufikia muafaka licha ya kuwepo kwa sehemu kubwa ya waliohusika na mchezo kati ya Kagera Sugar na African Lyon, ambao ndiyo mchezo unaobishaniwa kuwa mchezaji Mohamed Fakhi alipewa au hakupewa kadi ya njano.

Baadhi ya wahusika hao ni pamoja na viongozi wa timu zote tatu (Kagera, Simba na African Lyon), waamuzi wote wa mchezo ule, mchezaji mwenyewe wa Kagera Mohamed Fakhi na wengineo

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa TFF, Celestine Mwesigwa, Kamati hiyo inahitaji ushahidi zaidi ili kulimaliza suala hilo, na amesema kikao kingine kitafanyika kesho Jumatano Aprili 19 kuanzia saa 6 mchana.

"Hili suala hi la kisheria kwahiyo linahitaji ushahidi zaidi, kuna watu wanadhani kamati hii inakaa ili kupindua maamuzi ya kamati ya saa 72, lakini kimsingi jukumu la kamati hii ni kutafsri sheria siyo kubadili maamuzi ya kamati nyingine" Amesema Mwesigwa

Mwesigwa amesema pia kuwa kikao hicho kimejadili suala la mchezaji wa Ludovic Venance aliyelalamikiwa kuwa na utata kwenye usajili wake katika klabu ya African Lyon, ambapo amesema kamati imemuidhinisha mchezaji huyo kuchezea African Lyon akitokea Mbao FC.

Amesema Kamati hiyo imebaini kuwa usajili wake ulikuwa na utata uliosababishwa na baadhi ya viongozi ambao watachukuliwa hatua huku timu ya African Lyon ikipigwa faini ya shilingi laki 5.

Mwesigwa hajazungumzia malalamiko ya Yanga ya kudai ushindi wa mchezo uliowakutanisha wao na African Lyon ambao mchezaji huyo alicheza, na baadaye Yanga kulalamika kuwa Ludovic hakuwa mchezaji halali wa Africa Lyon.

Katika mchezo huo, Yanga ilitoka sare ya bao 1-1 na African Lyon