Ijumaa , 20th Oct , 2017

Klabu ya Roma imeshitakiwa na UEFA baada ya baadhi ya mashabiki wake kusikika wakiimba  nyimbo zenye ujumbe wa ubaguzi wa rangi kwa kumwita Nyani mlinzi wa Chelsea Antonio Rudiger.

Mchezaji huyo wa kimataifa wa Ujerumani aliingia dakika ya 77 kwenye mchezo wa Ligi ya Mabingwa siku ya Jumatano ambapo mchezo huo ulimalizika kwa matokeo ya 3-3 kwenye dimba la Stamford Bridge.

Kesi hiyo itasikilizwa na kutolewa maamuzi Novemba 16 mwaka huu na Kamati ya UEFA ya Udhibiti wa Maadili na Nidhamu.

Rudiger, mwenye umri wa miaka 24, amehamia Chelsea kutoka Roma kwenye usajili wa majira ya joto mwaka huu. Kabla ya kuhamia Uingereza kwa gharama ya £ 29m, Rudiger alisema ubaguzi wa rangi katika mechi za mpira wa miguu ni tatizo kubwa nchini Italia.