Jumatatu , 20th Nov , 2017

Mechi za wikiendi hii za Ligi Kuu ya soka Tanzania Bara zinazozihusu Simba na Yanga zitachezwa Uwanja wa Azam FC Complex, Chamazi mjini Dar es Salaam.

Hiyo inafuatia uwanja wa Uhuru kuwa na matumizi mengine ya kijamii na wakati huo huo, Uwanja wa Taifa bado haujaruhusiwa kwa matumizi kufuatia ukarabati wa eneo la kuchezea.

Yanga watakuwa wenyeji wa Tanzania Prisons ya Mbeya Jumamosi wakati Simba wataikaribisha Lipuli ya Iringa Jumapili katika michezo ya Ligi Kuu raundi ya 11.

Taarifa kutoka bodi ya Ligi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), imesema kwamba kwa sababu hiyo mechi hizo zimepelekwa Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.

Baada ya mechi 10 za awali, Simba SC wapo kileleni kwa pointi 22, sawa na Azam FC wanaokaa nafasi ya pili kwa kuzidiwa wastani wa mabao, wakati mabingwa watetezi, Yanga SC wapo nafasi ya tatu wakiwa na pointi 20.