Ijumaa , 17th Nov , 2017

Klabu ya soka ya Singida United imeibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Lipuli FC kwenye mchezo uliomalizika jioni hii kwenye uwanja wa Namfua mjini Singida.

Matokeo hayo ya ushindi kwenye mchezo wa raundi ya 10 yanaifanya klabu hiyo iliyopanda daraja msimu huu kufikisha alama 17 na kupanda hadi nafasi ya 5 kwenye msimamo wa ligi.

Ushindi wa leo ni wa kwanza kwa timu hiyo kwenye uwanja wake wa nyumbani wa Namfua ambao iliufungua Novemba 4 kwenye mchezo dhidi ya Yanga ambapo timu hizo zilitoka sare ya 0-0.

Lipuli FC imesalia katika nafasi ya saba na alama zake 13 ikisubiri matokeo ya baadhi ya michezo ya kesho na jumapili. Vinara wa ligi hiyo Simba SC kesho watachuana na Tanzania Prisons wakati mabingwa watetezi Yanga SC watacheza na Mbeya City.