Jumatatu , 27th Mar , 2017

Washambuliaji wawili ambao ni kipenzi cha watanzania wengi wanapokuwa katika vilabu vyao vya Simba na Yanga Amis Tambwe na Laudit Mavugo kesho watakuwa maadui wakubwa kwa watanzania watakapoiongoza timu yao ya Taifa ya Burundi dhidi ya Taifa Stars

Taifa Stars ya Tanzania kesho Machi 28, 2017 saa 10:00 jioni inaingia tena Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, kucheza na timu hiyo ya Burundi maarufu kwa jina la Intamba Murugamba katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa, kwa mujibu wa kalenda ya wiki ya mechi za kimataifa ya FIFA.

Tayari Intamba Murugamba wametua nchini tangu jana Jumapili saa 4.30 asubuhi na kufikia Hoteli ya De Mag iliyoko, Kinondoni, Dar es Salaam na jioni yake walifanya mazoezi kwenye Uwanja wa Karume, Ilala jijini. Leo Jumatatu.inafanya mazoezi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Ndani ya kikosi hicho wamo washambuliaji wawili wanaotamba katika klabu za Simba na Young African za Dar es Salaam. Nyota hao ni Amisi Tambwe wa Young Africans na Laudit Mavugo wa Simba.

Wakati Mavugo ni mshambuluaji, anatarajiwa kuwa na wakati mgumu mbele ya walinzi mahiri ambao pia wako Simba kama vile Abdi Banda na Mohammed Hussein wakati Andrew Vicent anayetoka Young African atakuwa kisiki kwa Tambwe wanayecheza naye timu moja kama makocha watawapanga.

Taifa Stars Vs Botswana

Kwa upande wake, Mayanga alifurahishwa na ushindi wa Jumamosi iliyopita dhidi ya The Zebras ya Botswana na hivyo amehimiza Watanzania kujitokeza kwa wingi katika mchezo wa kesho.

Katika kuunga mkono wito wa Kocha Mayanga, TFF imebakiza viingilio vya mchezo huo kuwa sawa na vile vya Jumamosi iliyopita kwani katika mzunguko ambao unachukua mashabiki wengi kiingilio kitakuwa ni Sh 3,000.

Kwa upande wa VIP “A” Kiingilio kitakuwa ni Sh 15,000 wakati VIP “B” na VIP “C” kiingilio kitakuwa ni Sh 10,000. Viingilio hivyo vimelenga kuwaalika Watanzania wengine kwenda uwanjani.