Ijumaa , 22nd Oct , 2021

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Kassim Majaliwa ameisisitiza Wizara ya Sanaa,  Utamaduni na Michezo kuhakikisha timu ya Biashara United Mara inasafiri kwenda Libya kwa ajili ya kucheza mechi ya marudiano dhidi ya Al Alhi Tripoli kwenye la Kombe la Shirikisho Afrika

(Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Kassim Majaliwa alipokuwa akihutubia kwenye usiku wa hafla ya tuzo usiku wa jana.)

Waziri Majaliwa ameyazungumza hayo alipokua anatoa hotuba yake katika hafla ya utoaji wa tuzo za Ligi Kuu msimu uliopita iliyofanyika usiku wa jana. Waziri Mkuu amesema itakuwa jambo la kushangaza kuona Biashara United haijaenda Libya kwa ajili ya mechi hiyo ya marudiano kisa kukosa pesa.

"Mkurugenzi Baada ya shughuli hizi mkae mjipange biashara iondoke nchini na tunaamini watashinda. Timu iende ikashindwe huko lakini naamini itashinda. Mhakikishe timu inaenda kule Libya," alisema Waziri Mkuu

Waziri Mkuu Majaliwa alisema hilo litachochea ushindani katika Ligi Kuu kwani timu zitapata ari na moyo wa kupambana kupata nafasi ya kuwakilisha nchi kimataifa.

Katika mchezo huo wa marudiano, utakaochezwa jijini Benghazi, Jumamosi jioni, Biashara United inahitaji ushindi au sare ya aina yoyote ili iweze kutinga hatua ya mwisho ya mchujo ya mashindano hayo

Katika mchezo wa kwanza hapa Dar es Salaam, Biashara United iliibuka na ushindi wa mabao 2-0 yaliyofungwa na Deogratias Mafie na Atupele Green