Jumamosi , 14th Oct , 2017

Kocha wa Real Madrid Zinedine Zidane amesema hawezi kuifundisha Barcelona kwani moyo wake ni mweupe na daima utakuwa hivyo.

Zidane ameyasema hayo mapema leo kwenye kikao cha maandalizi ya mechi ya ligi kuu ya Hispania La Liga dhidi ya Getafe utakaopigwa jioni.

Zidane ambaye leo anatimiza mechi 100 akiwa kocha mkuu wa Real Madrid aliulizwa endapo siku moja atapokea ofa ya kuwafundisha mahasimu wao Barcelona, Zidane alisema hawezi kufanya hivyo kwani yeye ni Madrid na atabaki kuwa hivyo.

“Moyo wangu ni mweupe na daima utabaki hivyo, sifikirii kufundisha kwingine kwasasa nipo hapa na nitaendelea kuwa hapa”, amesema Zidane.

Katika mechi zake 99 ambazo ameifundisha Real Madrid tayari ameiwezesha kushinda mataji 7 ikiwemo ubingwa wa UEFA mara mbili mfululizo. Real Madrid ipo nafasi ya 5 ikiwa na alama 14, ikizidiwa alama 5 na wapinzani wao Barcelona ambao wana alama 19 kileleni.