Jumapili , 22nd Jul , 2018

Polisi wilayani Serengeti Mkoa wa Mara wamewatia mbaroni watu kumi kwa kosa la kuwakuta na nyara za Taifa kinyume cha sheria.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Mara, Juma Ndaki

Kamanda wa Polisi mkoa huo, Juma Ndaki amesema watuhumiwa hao 10 wamekutwa na vipande 531 vya nyama kavu za wanyama pori, mikia 24 ya nyumbu, mikia 12 ya pundamilia, nyaya 75 za kutegea, mapanga mawili, visu viwili, dumu nane za maji na baiskeli 10.

Akizungumza na Wanahabari, Kamanda Ndaki amesema mzigo huo ulikamatwa kwenye kambi yao ya ujangili eneo la Togoro ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kwa ushirikiano wa askari wa Hifadhi hiyo na Polisi wilayani humo.

Watuhumiwa wote hao ni wakazi wa kata za Nyambureti na Nyamatare wilayani Serengeti.