Jumatatu , 17th Jun , 2019

Mkuu wa wilaya ya Arumeru Ndugu Jerry Muro, ametoa muda wa mwezi mmoja kwa wananchi wilayani humo kuachana na suala la kuajiri watoto wadogo kwaajili ya kufanya kazi za ndani.

Mkuu wa wilaya ya Arumeru Ndugu Jerry Muro

Akiongea siku ya maadhimisho ya mtoto wa Afrika, Muro amewataka watu wote wanaowatumikisha watoto wadogo kazi za majumbani (House Girls) kuhakikisha wanawapaleka watoto hao shule au kuwarejesha kwao.

''Kama unajua una mtoto ambaye unamtumikisha kwa kazi za ndani na hajafika umri wa miaka 18, naomba umpeleke shule na kama hilo litashindikana naomba umrudishe kwako au niletee mimi ofisini kwangu tunao utaratibu mzuri wa kuwahudumia'', amesema.

Ameongeza kuwa endapo watoto hao watapelekwa katika ofisi za Mkuu wa wilaya ya Arumeru, idara ya ustawi wa jamii italazimika kuwapeleka katika maeneo maalum ya kuwalea ili kuweza kupata fursa ya elimu na malezi bora.