Jumapili , 14th Jul , 2019

Rais wa Tanzania Dkt. John Magufuli, amemteua kuwa Mkuu wa Wilaya ya Tunduru aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi wa Chama Cha wananchi (CUF) Julius Mtatiro, ambaye alitangaza kuhamia CCM kutokana na chama chake cha CUF kukabiliwa na migogoro ya kiuongozi.

Uteuzi wa Julius Mtatiro umetangazwa na Rais wa Magufuli leo asubuhi ya Julai 14, 2019, akiwa wilayani Chato kwa mapumziko binafsi, ambapo uteuzi huo unatarajia kuanza mara moja kuanzia leo Jumapili.

Kabla ya Mtatito kushika nafasi hiyo, awali ilikuwa ikishikiliwa na Juma Homera ambaye kwa sasa ni Mkuu wa Mkoa wa Katavi.

Akizungumzia uteuzi huo, Julius Mtatiro amesema kuwa, "nimezipokea taarifa nikiwa safarini tena, tena nimezipokea kwa mshtuko sana, kwa sababu sikutarajia kwamba naweza kuteuliwa na Rais, unajua ukiteuliwa halafu hukuwa unatarajia unapata mshtuko sana."

"Ila ukimaliza kupokea kwa mshtuko hizo taarifa inabidi ukubaliane nazo tu, kwa sababu ni kazi ya umma na hakuna budi kuitumikia", amesema Mtatiro.

Agosti 11, 2018 kwenye mkutano wake na waandishi wa habari, Mtatiro alitangaza kujiondoa Chama Cha Wananchi CUF, kwa kile alichokieleza alikosa nafasi nzuri ya kuwatumikia Watanzania na kumaliza matatizo yao.

Sikiliza mahojiano kamili na Mtatiro, Bonyeza hapo chini