Jumanne , 11th Dec , 2018

Aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Kasulu Mjini ambaye kwa sasa ni Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu, Moses Machali, amesita kuzungumzia safari yake ya kuelekea kwenye uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020 na kubainisha kuwa hajui kama atawania nafasi yeyote.

Makao Makuu madogo ya CCM Dar es salaam.

Machali amesema hawezi kuzungumzia nafasi ya kurudi bungeni kwa sasa kutokana na kubanwa na taratibu za chama chake ambazo zinamkataza mwananchama wa kawaida kuonesha nia ya kuwania nafasi yeyote wakati kuna viongozi husika.

"Kuhusu suala la kugombea tena ubunge kupitia CCM kwa sasa sina cha kusema, sitaongea kwa sasa kwa sababu nitakuwa nimekiuka misingi ya chama, kwa hiyo nahifadhi maneno yangu," amesema Machali.

"Hata uniulize kwa namna gani, msimamo wangu kugombea nafasi yeyote 2020 bado nitaendelea kutosema chochote, mpaka wakati muafaka utakapowadia." ameongeza Machali.

Akizungumza na www.eatv.tv, oktoba 31, 2018 David Kafulila ambaye alihamia CCM kutoka CHADEMA alisema “suala la kugombea au kutogombea ubunge ni muda tu ila kwa sasa hivi ninachoweza kuzungumza ni kwamba nafurahia kufanya kazi."

Moses Machali aliteuliwa na Rais Magufuli, Julai 28 mwaka huu kuwa Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu pamoja na makada wengine waliohama kutoka upinzani na kujiunga na CCM, akiwemo Mkuu wa wilaya ya Dodoma Mjini, Patrobas Katambi na David Kafulila ambaye ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Songwe.