Ijumaa , 15th Mar , 2019

Askari Polisi mkoani Ruvuma, amekutwa amekufa kwenye baa moja inayopatikana katikati ya mji wa Songea mkoani Ruvuma.

Akithibitisha taarifa za kifo hicho, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma, Simon Marwa amesema askari aliyefariki anajulikana kwa jina la Donald Motoulaya (29), mzaliwa wa Mtwango mkoani Njombe, na alifariki kutokana na maradhi ya presha na si ulevi kama ilivyosemekana.

Kamanda Marwa amesema kwamba Donald alikutwa amelala kwenye kochi la bar hiyo, baada ya kuteleza alipokuwa akiingia na kumueleza kuwa alikuwa akijisikia vibaya.

RPC asimulia

Si kweli kuwa alikuwa amelewa, alikuwa  ameenda pale bar, wakati anaingia kateleza akaanguka, hata ukimuangalia shavuni ana mkwaruzo hivi, muhudumu mmoja anaitwa Jovina akamuuliza vipi akasema najisikia kukosa hewa, akamsaidia kumtoa nje, kumbe baadaye akaingia ndani akaa kwenye sofa akalala, alivyolala watu hawakujua kama kuna mtu, asubuhi wanakuja kufanya usafi ndio wakamuona, kumkimbiza hozpitali Daktari akasema ameshafariki, na kilichomuua kwa mujibu wake ni kushuka kwa presha”, amesema Kamanda Marwa.

Kamanda Marwa amesema kwamba mwili wa askari huyo tayari umeshasafirishwa kwenda Mtwango kwa mazishi ambayo yanafanyika mchana wa leo Machi 15.

Kwa mujibu wa Kanda Marwa, askari huyo hakuagiza kinywaji chochote, kutokana na taarifa walizozipata kutoka kwa wahudumu wa bar hiyo, pia wengine hawakujua kama yumo ndani.