Wabunge wa CHADEMA, Anthony Komu (kushoto) na Saed Kubenea (kulia)
CHADEMA wameazimia kuwavua nyadhifa zote za uongozi ndani ya chama
Akizungumza na wanahabari, Naibu Katibu Mkuu Bara John Mnyika amesema kuwa, Kamati Kuu ya chama iliwaita wabunge hawa kuja kujieleza juu ya tuhuma ya utovu huo wa nidhamu, na walifika kujieleza, na walikiri kwamba ni sauti zao.
Mnyika amesema Kamati kuu imewakuta na hatia, imefanya maamuzi ya adhabu juu yao, "mosi imefikia uamuzi wa kuwapa onyo, pili imewataka waandike barua ya kuomba radhi kwa chama., tatu Kamati kuu ikafikia uamuzi wa kuwaweka kwenye uangalizi kwa miezi 12, na nne ikafikia uamuzi wa kuwavua nafasi zao zote za uongozi ndani ya chama na kubaki na ubunge"
Pia wabunge hao Antony Komu na Saed Kubenea ambao pia wamehudhuia mkutano huo, wametakiwa kujitokeza mbele ya umma na kuomba radhi.
Kubenea na Komu sauti zao zilianza kuzagaa Jumapili ya Oktoba 14, kwenye mitandao ya kijamii ambapo moja kati ya mazungumzo yao walidai kuwa Meya Boniphace Jacob wa Ubungo kupitia CHADEMA ndiye mpambe wa mwenyekiti wa chama hicho taifa, Freeman Mbowe hivyo wanatafuta namna ya kumuondoa na kukihama chama.