Jumapili , 22nd Jul , 2018

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimepatwa na kigugumizi kutaja sababu ya kuwavua uanachama madiwani wake watatu siku ya jana (Jumamosi, Julai 22) na kubaki wakisisitiza ni utovu wa nidhamu.

Akizungumza na www.eatv.tv, Mkurugenzi wa Itifaki na Mawasiliano ya Mambo ya Nje wa CHADEMA, John Mrema amewataja madiwani waliovuliwa uanachama kuwa ni Geofrey Kajigili wa Kata ya Sisimba, Newton Mwatujobe wa Kata ya Manga na Humphrey Ngalawa wa kata ya Iwambi Jijini Mbeya huku akishindwa kutaja sababu iliyopelekea maamuzi hayo kufanyika kwa kudai suala hilo lipo kwenye uchunguzi.

 "Ni kweli tumewavua uanachama Madiwani hao watatu kutokana na vitendo vyao vya utovu wa nidhamu walivyovionyesha ambavyo vinakinzana na chama chetu. Siwezi kusema nini hasa wamekifanya kwa kuwa jambo hilo kwa  sasa lipo kwenye Kamati Kuu linasubiriwa kufanyiwa maamuzi", amesema Mrema.

 Pamoja na hayo, Mrema amesema kwa sasa hawezi thibitisha jambo lolote kuhusu diwani Kajigili kudaiwa kumpigia kampeni hadharani Naibu Spika Dkt. Tulia Ackson, kwamba anastahili kuwa Mbunge wa Mbeya mjini mpaka pale Kamati Kuu itakapotoa maamuzi yao juu ya uchunguzi ambao wanaufanya.