Ijumaa , 12th Oct , 2018

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi CCM, Dkt Bashiru Ally amevikosoa vyama vya siasa nchini kwa kile alichokidai vyama vingi kukosa nidhamu katika kusimamia wanachama na misingi ya sera zake kunakosababishwa na viongozi waliopewa dhamana.

Dkt Bashiru ametoa kauli hiyo wakati akichangia kwenye mjadala wa miaka 19 ya kumbukumbu ya  Mwalimu Julius Nyerere iliyofanyika Chuo Kikuu cha Dar es salaam, ambapo viongozi mbalimbali akiwemo Zitto Kabwe, Nape Nnauye, Dkt Vincent  Mashinji wameshiriki.

Akichangia kuhusu suala la nidhamu kwenye vyama vya siasa, Dkt Bashiru amesema "vyama vyetu havina nidhamu, wanachama hawana nidhamu, wanachama wetu hawahudhurii vikao, suala la nidhamu ni jambo kubwa sana la kuzingatia."

"Suala jingine vyama vyetu vingi ni tegemezi, vinategemea pesa kutoka kwa baadhi ya mabeberu, bila vyama hivi kuvijenga kujiendesha kwa wanachama na vyanzo vya ndani kuna hatari matajiri wakaviendesha tuache kuendekeza watu wa nje waongoze vyama vyetu", ameongeza kiongozi huyo.

Aidha Dkt Bashiru amesema miongoni mwa hofu zinazowakabili wananchi walio wengi nchini ni hofu ya kukosa huduma za kijamii, huku akipinga baadhi ya hoja zinazotangazwa na watu aliowaita wasiokuwa na uadilifu.