Jumapili , 2nd Aug , 2020

Upokeaji wa hati katika viunga vya Ikulu jijini Dar es Salaam ulianza rasmi majira ya Saa 9:00 Alasiri, ambapo Mh. Rais John Magufuli amepokea hati za Mabalozi wateule wawili.

Rais Magufuli akiwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Profesa Palamagamba Kabudi katika picha ya pamoja na Balozi wa Marekani hapa nchini Donald John Wright Ikulu Dar es Salaam.

Mabalozi hao ni Mhe. Nguyen Nam Tien Balozi Mteule wa Vietnam Nchini Tanzania, pamoja na Mhe. Donald John Wright Balozi mteule wa Marekani hapa nchini.

Baada ya hati za Mabalozi wateule kupokelewa, sasa wanatambulika rasmi kama mabalozi kamili kwa niaba ya nchi zao hapa nchini. 

Vietnam imekuwa na uhusiano wa kidiplomasia na Taifa la Tanzania kuanzia mwaka 1965 ikiwa ni takribani miaka 55, pamoja na mambo mengine taifa hilo limewekeza katika sekta ya mawasiliano hapa nchini ambapo wamiliki wa mtandao wa Halotel wanatokea taifa hilo.

Kwa takribani miaka mitano Marekani haikuwa imemteua balozi wa taifa hilo kuja nchini, ambapo balozi wa mwisho alikuwa Mark Childress aliyemaliza muda wake mwaka 2016 na kufuatiwa na Kaimu Balozi Inmi Patterson ambaye alimaliza muda wake mwezi juni mwaka huu.

Rais Magufuli akiwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof Palamagamba Kabudi katika picha ya pamoja na Balozi wa Vietnam nchini Nguyen Nam Tien baada ya kuwasilisha Hati zake za Utambulisho katika hafla iliyofanyika Ikulu Dar es Salaam

Kwa upande wa Balozi huyo mgeni Mhe. Donald, amewahi kufika nchini miaka 33 iliyopita ambapo alikuwa amekuja kutibu watoto huko visiwani Zanzibar.

Aidha mahusiano ya Tanzania na Marekani yanatarajiwa kuimarika zaidi, kwani takwimu zinaonesha kuwa miradi ya wawekezaji wa Marekani inafikia 3179 ikiwa imetengeneza ajira 550,000 na mauzo ya Tanzania nchini Marekani kwa mwaka jana ilikuwa ni Shillingi Biliioni 119. 

Huku taifa hilo likiwa limetoa zaidi ya dola million 600 ambazo zimeelekezwa katika sekta tofauti za kimkakati kama afya, kilimo na elimu.