Alhamisi , 11th Apr , 2019

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Humphrey Polepole, amesema kuwa kuwa viongozi ambao hawafanyi vizuri katika majukumu yao hawatopata ridhaa ya kugombea uchaguzi ujao.

Polepole akizungumza.

Polepole ametoa kauli hiyo leo Aprili 11, akiwa katika ziara ya kikazi wilayani Ubungo jijini Dar es salaam, ambapo anafuatilia utekelezaji wa miradi kwa mujibu wa Ilani ya chama tawala.

"Lazima mfahamu kuwa wenyeviti wa serikali za mitaa ambao hawafanyi kazi vizuri kwa mujibu wa sheria, hatutawapa nafasi tena katika uchaguzi huu wa 2019", amesema Polepole.

Akizungumzia watumishi wa umma wasio ifahamu ilani ya chama tawala amesema kuwa, "huwezi kuwa unafanyakazi msikitini halafu hujui hata kutamka Asallamu Alleikum, haiwezekani mtu anafanyakazi ya Serikali ya CCM na hataki kuijua Ilani ya CCM, sera zake na taratibu zake".

Sanjari na hayo Polepole amedai kuwa moja kati ya sehemu ambayo CCM inaitazama kwa macho manne ni pamoja na Ubungo, hivyo ni lazima kuimarisha chama katika eneo hilo.