Alhamisi , 7th Nov , 2019

Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Selemani Jafo, amezitaka Kamati za Rufaa kushugulikia malalamiko ya wagombea watakaokata rufaa na kutoa maamuzi sahihi ili kuufanya uchaguzi wa Serikali za Mitaa kuwa wa amani na haki.

Waziri Jafo ametoa kauli hiyo akiwa mkoani Iringa, ambapo amesema amepokea malalamiko mengi kutoka kwa wagombea hasa wa upinzani kwa kile kinachoelezwa kuwa hawajatendewa haki katika zoezi hilo.

"Nendeni mkafanye kazi kwa weledi, sitaki nyinyi muwe watu mtakaopitisha yaliyofanyika kule chini, naombeni mkaangalie yale malalamiko ya mtu anayelalamika muangalie mufanye maamuzi bila kufungwa na mtu yeyote." amesema Jafo.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Iringa Ally Hapi, amesema anataarifa ya Mitaa 46, ambayo vyama vya upinzani havikuchukua fomu kabisa.

Novemba 24, 2019, Watanzania wanatarajia kushiriki zoezi la kupiga kura kwa kuwachagua viongozi wa Serikali za Mitaa.