Jumanne , 12th Nov , 2019

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, amesema kuwa hapendi kuwapongeza sana wateule wake, kwakuwa hatua hiyo ilimfanya achukiwe na viongozi wenzake alipokuwa Waziri wa Ujenzi.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli.

Rais Magufuli ametoa kauli hiyo leo Novemba 12, 2019, wakati akizungumza kwenye uzinduzi wa Kitabu cha Rais Mstaafu Benjamin Mkapa, ambapo amesema anamshukuru kiongozi huyo kwa kuwa shujaa katika uongozi wake licha ya changamoto alizozipitia.

"Akifurahia jambo hafichi furaha yake na akichukia hafichi chuki yake, nakumbuka Mzee Mkapa pale tulipofanya kazi vizuri, alipata furaha sana kwenye kazi za barabara mpaka akatamka kuwa mimi ni Askari wake namba moja, suala hilo liliniletea matatizo kwangu, ilifikia hatua baadhi ya Mawaziri wa ngazi za juu walianza kunichukia, lakini ilifika hatua na kuniwekea sumu almanusura ichukue uhai wangu, nilipomfuata akaniangalia kwa jicho la Baba na Mama" amesema Rais Magufuli.

Aidha Rais Magufuli ameongeza kuwa, "Hilo suala lilinifunza sana hata mimi sasa hivi siwasifii sana wateule wangu, kwa sababu yasije yakawakuta yaliyotaka kunikuta mimi".

Kitabu hicho kilichozinduliwa na Rais Mstaafu Mkapa kinatambulika kwa jina Maisha yangu, Lengo Langu. 'My Life, My Purpose.'