Jumapili , 10th Nov , 2019

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Anna Mghwira, amesema watu kadhaa wanashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani humo, kwa tuhuma za kuchoma moto ofisi ya Kata ya Soweto iliyopo Moshi.

Awali tukio hilo liliripotiwa kufanywa na watu wasiojulikana, ambapo  wamechoma moto ofisi ya Afisa Mtendaji wa Kata ya Soweto usiku wa kuamkia leo, Novemba 10, 2019, ambapo pia wamechoma nyaraka zilizokuwa ndani ya ofisi hizo.

Mkuu wa Mkoa Anna Mghwira, amesema kuwa moto huo ulianza majira ya saa 7 usiku, na baada ya moto huo kuwaka majirani waliokuwa karibu na ofisi hiyo walianza kuuzima na baadaye kutoa taarifa polisi.

Aidha Anna Mgwhira amewataka wananchi kuwa watulivu wakati vyombo vya ulinzi na usalama vikiendelea na uchunguzi.