Jumatatu , 16th Jul , 2018

Waziri wa Mambo ya Ndani Mhe. Kangi Lugola ametoa siku zisizozidi kumi kwa Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya vitambulisho NIDA, akiwa na kampuni ya Iris Dilham kufika ofisini kwake mjini Dodoma ili kueleza sababu ya kutofika kwa mtambo wa kuchapisha vitambulisho mpaka sasa.

Waziri wa Mambo ya Ndani Mhe. Kangi Lugola

Agizo la Mh. Lugola linakuwa ni utekelezaji wa miongozo aliyopatiwa na Rais Magufuli siku alipomuapisha kuwa Waziri wa Mambo ya ndani baada ya kutengua uteuzi wa Dkt. Mwigulu Nchemba.

Wakati akitoa muongozo wa maeneo sugu ndani ya Wizara ya Mambo ya Ndani, Julai 2 Rais Magufuli alisema "Kuna suala la NIDA, mambo ni hovyo. Kuna pesa zilichezewa, kuna vifaa viliagizwa na havikufika. Tumewachukulia hatua lakini waliofanya mambo hayo mpaka leo hatua gani wamechukuliwa? Je, pesa hizo zimerudishwa? Kasimamie hayo mambo," Rais Magufuli.

Mhe. Lugola amesema hayo baada ya kutembelea Ofisi ya Uzalishaji vitambulisho hivyo kilichopo Kibaha, mkoani Pwani na kutoridhishwa na kazi ya utoaji wa vitambulisho kwa wananchi, zoezi ambalo linaendelea kufanywa na NIDA katika maeneo mbalimbali nchini.

Waziri huyo amesema kuwa mpaka sasa kuna dalili za kuwa kampuni hiyo iliyopewa tenda imeshindwa kuleta mtambo huo hivyo atahitaji maelezo ya kina kuhusiana na hilo kabla hajachukua maamuzi mengine.

"Dalili zinaonyesha kwamba kampuni ya Iris Dilham haina mpango wa kutuletea huo mtambo. Sasa kama hawana mpango ni vyema wakatueleza fedha zetu ziko wapi. Nakuagiza Mkurugenzi Mkuu nataka nikiwa Dodoma Julai 25 mwaka huu majira ya saa nne mfike ofisini kwangu ukiwa na hao wenye kampuni ya Iris, na kwa kuwa wameonyesha kushindwa waje na hizo pesa in 'advance' kabisa ili kusudi tukazihifadhi benki tena tutapeleka na 'escort' ya juu. Ztafanyiwa shughuli nyingine. Hatuwezi kucheza na pesa za watanzania " amesema Waziri Lugola.

Msikilize hapa chini Mh. lugola akitoa maagizo.