Jumamosi , 13th Oct , 2018

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, amesema Jeshi la polisi linaendelea na mchakato wa kumtafuta mfanyabiashara maarufu Mohammed Dewji "Mo Dewji" aliyetekwa siku ya Alhamis Oktoba 11,2018 jijini Dar es slaam.

Mohammed Dewji kushoto na Kangi Lugola

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake leo, Kangi amesema takribani watu 20 wanashikiliwa na jeshi la polisi ili kusaidia kutoa ushirikiano wakati wakiendelea kuwasaka watu wote waliohusika na tukio la utekaji ikiwemo kumpata Dewji mwenyewe.

''Niwahakikishie watanzania, jeshi la polisi linaendelea kushughulikia tukio la kutekwa kwa Mohamedi Dewji, likiwasaka waliomteka na tutahakikisha wanapatikana, ambapo hadi sasa navyozungumza takribani watu 20 wanashikiliwa na jeshi la polisi kwa mahojiano'', amesema.

Mh. Lugola pia amemtaka IGP Simon Sirro kutoa maelekezo kwa askari wake, kuwaachia ndani ya saa 24 watu wanaowashikilia kwa uchunguzi kuhusiana na kutekwa kwa Mohammed Dewji mara baada ya kuwahoji na kubaini wahusika au hawana taarifa kamili.

Aidha akisoma taarifa ya matukio ya uharifu yaliyotokea nchini tangu mwaka 2016, Kangi amesema jeshi la polisi linaendelea kuwashikilia watuhumiwa wa matukio ya kiharifu na kuwataka wananchi kuacha minong'ono kwamba serikali na vyombo vya usalama havifanyi kazi ipasavyo.

Mwaka 2016 Watu 5 kati ya 9 waliokuwa wametekwa walipatikana wakiwa hai, huku watu 27 waliotekwa  mwaka 2017, 22 wamepatikana huku watatu wakiwa hawajapatikana.

Aidha takwimu za watoto walioripotiwa kupotea kuanzia Januari hadi Oktoba mwaka huu ni 21, ambapo watoto 17 wamepatikana wakiwa hai na watoto 4 hawajapatikana hadi sasa.