Jumatatu , 14th Mei , 2018

Mkuu wa Magereza ya Mkoa wa Dar es salaam, ACP Augustino Mboje amesema muigizaji wa filamu nchini Elizabeth Michael maarufu kama Lulu anaweza kurudi gerezani endapo ataonesha mwenendo usioridhisha wakati ambao atakua chini uangalizi

ACP Mboje amesema hayo leo Mei 14, 2018 alipokuwa anaongea na vyombo vya habari kuelezea sababu za msanii huyo kutoka kabla ya muda kifungo kuisha ambapo amedai kuwa Lulu amenufaika na msamaha wa Rais Magufuli aliotangaza katika sherehe za sikukuu ya Muungano Aprili 26, 2018 mjini Dodoma

“Kama atakiuka masharti ya kuchelewa, kuonesha tabia mbaya, mara siku moja moja haji, akawa haoneshi mwenendo mzuri, community worker atawasiliana na sisi (Lulu) atarudi gerezani kwa kupitia mahakamni kwasababu aliletwa na mahakama” amesema ACP Mboje

Awali ACP Mbonje aliongeza kuwa msanii huyo asingeweza kutoka 26 April 2018 hata baada ya kupewa msamaha na Rais Magufuli kwasababu alikua hajatumikia robo ya kifungo chake ambacho kilikua kinaisha Novenba 12, 2018 baada ya msamaha huo.

Sambamba na hilo ACP Mbonje amedai kwasasa msanii Lulu bado ni mfungwa ila atatumikia kifungo chake nje ya gereza mpaka novemba 12, 2018 kwa kufanya huduma za kijamii.

Kwa mujibu wa sheria ya Mahakama kifungu na. 3 (2) (a) ya huduma ya jamii ya mwaka 2002 inatoa nafasi kwa mfungwa ambae kifungo chake hakijazidi miaka mitatu kutumikia kifungo chake nje ya gereza kwa kufanya kazi zisizo na malipo kwa manufaa ya jamii.

Novemba 13, 2017 Mahakama Kuu kanda ya Dar es salaam ilimtia hatiani msanii Elizabeth Michael (Lulu) na kumhukumu kifungo cha miaka miwili jela kwa kosa la kumuua bila kukusudia msanii mwenzake Steven Kanumba April 7, 2012 nyumbani kwa marehemu Sinza Jijini Dar es Salaam.