Jumanne , 25th Feb , 2020

Mbunge wa Bumbuli na aliyewahi kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira January Makamba, amesema kuwa idadi kubwa ya Watanzania wanatambua mchango wake katika suala zima la kutokomeza matumizi ya mifuko ya plastiki, hata kama viongozi wengine wasipotambua.

Mbunge wa Bumbuli, January Makamba

Hayo ameyabainisha leo Februari 25, 2020, kupitia ukurasa wake wa Twitter, wakati akimjibu mwananchi aliyehoji kauli ya Waziri wa sasa Azzan Zungu, aliyedai kuwa suala la mifuko hiyo lilisimamiwa na viongozi wa juu bila kumtaja Makamba.

"Waziri hayuko wrong ni kweli viongozi wetu hao walitusimamia kwenye suala hili, kuhusu kutambua mchango wangu, karibu Watanzania wote wameutambua na hao kwangu wanatosha, hofu yangu ni kama tutashindwa kusimamia mafanikio yaliyopatikana na mifuko ya plastiki ikarejea mitaani" ameandika Makamba.

Hivi karibuni mara baada ya kuteuliwa kushika nafasi hiyo, Waziri Zungu alisema kuwa licha ya Serikali kupiga marufuku ya matumizi ya mifuko ya plastiki, lakini mifuko hiyo imeanza kurejea tena sokoni.