Jumapili , 12th Aug , 2018

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Paul Makonda leo ameanza rasmi mpango wa kuviwezesha kiuchumi vilabu vya Jogging kwa kuvipatia mitaji ya kuwezesha kuanzisha miradi ya kujikwamua kiuchumi.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam akiwa anafanya mazoezi

Akizungumza wakati wa Bonanza la Vilabu vya Jogging Dar es salaam makonda ameanza kwa kukabidhi kitita cha zawadi ya shilingi milioni 10 kwa washindi wa makundi mbalimbali pamoja na kuahidi kukabidhi shilingi Million Saba kwa chama cha Jogging Temeke ili waweze kuwa na SACOS yao endapo atajiridhisha kuwa wamekidhi vigezo.

Aidha amesema anachokitaka kwa sasa ni kuona vilabu vya Jogging vinashiriki shughuli za uzalishaji Mali ili wajikwamue kiuchumi na wasipate muda wa kushiriki matukio ya uhalifu kama uporaji, ubakaji na matumizi ya dawa za kulevya.

Makonda amesema kila baada ya miezi miwili yatakuwa yakifanyika mabonanza makubwa ya Jogging hivyo amezitaka kila wilaya kujiandaa.

Pamoja na hayo amewataka vijana mkoani kwake kuchangamkia fursa zote halali zinazopatikana Dar es salaam kwakuwa mkoa huo Ndio chimbuko la mafanikio kwa wengi huku akiwahimiza kumtanguliza Mungu kwa kila jambo.

Hata hivyo mkuu huyo amewaomba Vijana wa Jogging kuwa mstari wa mbele kuwafichua wahalifu ili Dar es salaam iendelee kubaki kuwa jiji lenye amani na usalama wakati wote.