Jumatatu , 14th Sep , 2020

Msemaji wa wababe wa Mlandizi Pwani Ruvu Shooting Masau Bwire ameelezea kusikitishwa kwake na timu yake kufungwa na timu aliyoiita kuwa ni mbovu.

Msemaji wa wababe wa Mlandizi Pwani Ruvu Shooting Masau Bwire

Masau ametoa kauli hiyo hii leo alipozungumza na mwandishi wetu kwa njia ya simu akiwa njiani kurejea kutoka jijini Mbeya ambapo siku ya jana majira ya Saa 8:00 Mchana Ihefu FC waliwakaribisha Ruvu shooting katika muendelezo wa Ligi Kuu Tanzania VPL na wenyeji kujihakikishia ushindi mapema dakika ya 7 ya mchezo kupitia Enock Jiah

"Mechi ilikuwa ya kawaida na timu tuliyocheza nayo ilikuwa na kiwango chake kilikuwa cha chini sana mpaka kiasi cha kusema kwamba miongoni mwa timu mbovu msimu huu ni pamoja na Ihefu lakini ajabu, shangaa tukapoteza mchezo. Lakini tukaamini kwamba kwenye soka hayo huwa yanatokea usipotarajia unaweza kupata au kupoteza'', amesema.

Aidha, kuhusu uwanja waliochezea Masau amesema kuwa uwanja ulikuwa wakawaida na wao kama wazoefu wa Ligi Kuu hawawezi kushangazwa na hali hiyo uwanja na kusifu kuwa upo kwenye viwango vya kuchezewa Ligi Kuu.

Kwa upande mwingine lawama zake akazielekezea kwa waamuzi wa mchezo huo kuwa kulikuwa na changamoto hivyo kuwataka waamuzi wasiwe tofauti na matakwa ya sheria hali inayoweza kupelekea kupata washindi wasiostahiki.