Alhamisi , 2nd Apr , 2020

Jumla ya mashahidi wanane kati ya 10 wanaotarajiwa kutoa ushahidi katika kesi ya uchochezi inayomkabili Kiongozi wa Chama Cha ACT Wazalendo Zitto Kabwe, tayari wamekwishatoa ushahidi wao katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Jijini Dar es Salaam.

Kiongozi wa Chama cha ACT Wazalendo, Zitto Kabwe

Kesi hiyo ambayo inasikilizwa na Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo Huruma Shaidi, leo Aprili 2, 2020, imeendelea ambapo mashahidi watatu wametoa ushahidi wao na hivyo kufanya idadi ya mashahidi ambao wamekwishatoa ushahidi kufikia nane.

Mmoja wa mashahidi hao ameiambia Mahakama kuwa alitumiwa na vyombo vya usalama kuwatuliza wananchi, waliokuwa na hasira pamoja na kutumwa afanye uchunguzi ili kupatikana bunduki za Polisi zilizopotea.

Shahidi mwingine katika kesi hiyo ameiambia Mahakama kuwa, alishuhudia nyumba zikichomwa moto na Polisi katika eneo la Mpeta mkoani Kigoma.

Inadaiwa kuwa Oktoba 28, 2018, Zitto akiwa katika Ofisi za Makao Makuu ya chama hicho, jijini Dar es Salaam, alitoa kauli za uchochezi kupitia mkutano wake na waandishi wa habari, na miongoni mwa matamshi yaliyomtia matatani ni pamoja na kusema kuwa Jeshi la Polisi lilihusika kufanya mauaji kwa wananchi 100 mkoani Kigoma.