Jumapili , 10th Feb , 2019

Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimethibitisha Mbunge wake wa viti maalum kutokea Zanzibar, Zainab Mussa Bakari kupata ajali katika eneo la Dumila mkoani Morogoro alipokuwa akitokea Jijini Dodoma kuja Dar es salaam kufuatia kuahirishwa kwa vikao vya Bunge.

Gari la Mbunge lililopata ajali

Taarifa ya ajali hiyo imetolewa na Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa CHADEMA, Tumaini Makene akisema kuwa Mbunge huyo anatarajiwa kuhamishiwa hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa ajili ya kupatiwa matibabu zaidi.

"Mbunge wa CHADEMA (VM) Zanzibar, Bi. Zainab Mussa Bakari amepata ajali eneo la Dumila akitoka Dodoma leo, abiria wote 3 na dereva wamejeruhiwa."

"Baada ya kutibiwa kwa dharura Morogoro, sasa wanapelekwa Hospitali ya Taifa Muhimbili1 kwa uchunguzi na matibabu zaidi" ameongeza Makene

Mapema jana, mmoja wa viongozi wa juu wa chama hicho, Waziri Mkuu Mstaafu Fredrick Sumaye alihamishiwa hospitali ya Taifa Muhimbili kwa ajili ya matibabu zaidi baada ya kuzidiwa alipokuwa kwenye majukumu ya kikazi mkoani Tanga.