Jumatatu , 24th Jun , 2019

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Kangi Lugola ameeleza Serikali ina mpango wa kupeleka Maaskari wanawake katika baadhi ya Majimbo nchini kufuatia maombi yaliyotolewa na Wabunge wengi.

Waziri Lugola ametoa kauli hiyo Bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Geita Vijijini Joseph Kasheku (Musukuma), ambapo Kangi lugola alieleza anajua wanaume wengi huwa wanafurahia zaidi wakikaguliwa na Maaskari wanawake kuliko wanawake kukaguliwa na wenzao.

"Wapo Wabunge wengi wanaomba tuwapelekee Maaskari wanawake, ninajua wanapokuwa Maaskari wanawake ni faraja kwa wananchi, kwa sababu wao wanaruhusiwa kuwakagua hata wanaume, nimpe faraja Mbunge Musukuma tutawapelekea Askari wanawake." amesema Kangi Lugola

Awali akiuliza swali Mbunge Musukuma ameliza kuwa "nisikitike kwa majibu yaliyotolewa na Naibu Waziri sio sahihi, maeneo ya jirani wana askari wa kike nataka kujua ni lini Serikali itanipatia askari wanawake?"

Waziri Kangi : "ni kweli lazima Askari mwanamke ampekue mtuhumiwa wa kiume, na kama hakuna askari mwanamke uko utaratibu wa kutumia mgambo wanawake au mke wa askari ambaye yuko jirani, nimeshamuagiza wa Kamanda wa Polisi Geita apeleke askari wakike"

Kwa sasa Bunge linaendelea jijini Dodoma ambapo Wabunge wanajadili pamoja na kuingia kura Makadirio ya Mapato na Matumizi ya 2019/2020.