Ijumaa , 4th Dec , 2020

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi amesema kuwa serikali haitovumilia vifo vya akina mama wajawazito vinavyosababishwa na uzembe wa watumishi kazini.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi

Prof. Makubi amesema hayo akiwa anafungua kikao kazi cha timu ya uongozi wa afya ya Mkoa wa Mwanza kilichofanyika Wilayani Misungwi kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga.

“Vifo vya akina mama wajawazito havivumiliki tena kwa sasa hivi kwenye hii dunia ambapo tumeingia uchumi wa kati, ni lazima tutafute mbinu mpya na nzuri tuweze kuziendeleza na kuhakikisha kwamba ambaye amekuja kuleta maisha asifariki” amesema Prof. Makubi

Aidha Prof.Makubi ameongeza kuwa wataalamu wa afya wahakikishe wanadhibiti vifo si vya akina mama wajawazito pekee bali  hata vifo vya watoto wachanga wanaozaliwa vinapaswa vidhibitiwe huku akieleza kushangazwa kutokea kwa vifo vingi vya akina mama wajawazito kutokea katika vituo vya kutolea huduma za afya na sio kwenye jamii na kuwataka watumishi hao kujitafakari na kutatua changamoto.

Hata hivyo Prof. Makubi ametoa wito kwa mikoa mingine kabla mwezi Januari 2021 hujafika kuendeleze kile ambacho mkoa wa Mwanza imeanza kufanya kwa kufanya vikao vya tathmini na kuweka mikakati ya kudhibiti vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga.