Alhamisi , 6th Dec , 2018

Waziri wa Mifugo, na Uvuvi Luhaga Mpina amesema wizara yake haitamvumilia mwananchi yeyote ambaye atathibitika kuvunja sheria ambazo zinalinda rasilimali ikiwemo mifugo na uvuvi, lengo ni kuzifanya rasilimali hizo zimnufaishe kila mmoja.

Waziri wa Mifugo, na Uvuvi Luhaga Mpina

Waziri Mpina ametoa kauli hiyo wakati wa kikao cha tathmini ya operesheni Nzagamba kilichofanyika Jijini Dodoma ambapo alizungumza na baadhi ya watumishi wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi na kuwataka watumishi hao kuwa mstari wa mbele kuheshimu sheria.

"Mimi ni Waziri tu tena ni mtu mdogo sana na kama wanadhani mimi ni mdogo, basi wazifuate sheria na katiba ya nchi inayoelekeza nini cha kufanya kwenye ulinzi wa rasilimali za taifa, mtu binafsi akifanya magendo mimi na watumishi wangu hatutamkingia kifua," amesema Mpina.

"Kama wakidhani tena mimi mdogo, basi wamfuate Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzana kwa sababu yeye ndiyo mkubwa wa nchi, hakuna mtanzania ambaye sisi tutamkingia kifua akikamatwa nchi jirani amevunja sheria na atashughulikiwa kwa sheria za nchi hiyo, na mimi huku wanaotoka kule tutawashughulikia kwa mujibu wa sheria zetu," ameongeza.

Oktona 2017 Waziri Luhaga Mpina aliagiza kuchomwa moto kwa vifaranga zaidi ya 6000, kutokana na kuingia nchini bila kufuata sheria na taratibu za nchi ambazo zimekuwa zikikataza kuingia kwa mifugo ya aina hiyo kwa sababu ya ugonjwa wa mafua ya ndege.

Septemba 2018 Rais Magufuli akiwa Ukerewe alimpongeza Waziri huyo kwa hatua mbalimbali alizokuwa akizichukua katika kushughulikia masuala ya uvuvi haramu, pamoja na kupambana na kuingia kwa mifugo nchini bila ya kuwa na kibali.

"Ndiyo maana nilivyotoka pale (Wizara ya Mifugo na Uvuvi) niliamua kumtafuta Waziri ambaye ana maamuzi magumu kama mimi nikampata Luhaga Mpina, waache walaumu leo kesho watafurahi, Mpina wewe chapa kazi," alisema Rais Magufuli.