Jumatano , 3rd Jun , 2020

Jeshi la Polisi mkoani Kagera linamsaka kijana mmoja aitwaye Justine Joseph kwa tuhuma za kumpiga na kumuua mama yake mzazi, Theopista Joseph (72) mkazi wa kijiji cha Omukangando wilayani Kyerwa.

Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, Revocutus Malimi

Kijana Joseph amefanya mauaji hayo baada ya kumtuhumu mama yake kulewa kupita kiasi na kushindwa kumhudumia baba yake mzazi ambaye ni mgonjwa wa kiharusi.

Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, Revocutus Malimi amesema kuwa mtuhumiwa alimkataza mama yake kunywa pombe ili apate muda wa kumhudumia baba yake lakini hakusikia na badala yake amekuwa akimwacha nyumbani na kwenda kulewa, kitendo kilichomkasirisha mtuhumiwa na kuamua kumshambulia na kumsababishia kifo.

Mbali na tukio hilo kamanda huyo amesema kuwa polisi wanamshikilia Hamis Ruge maarufu kwa jina la Mashiku (36)mvuvi na mkazi wa Igabilo wilaya ya Bukoba, kwa tuhuma za kumuua mke wake, Happiness Ibrahimu, baada ya kutokea ugomvi baada ya mume kumzuia mke wake kulewa pombe bila mafanikio.