Jumapili , 13th Oct , 2019

Katika hali isiyokuwa ya kawaida mtoto mchanga amekutwa ametupwa jalalani katika kitongoji cha Majengo wilayani Manyoni mkoani Singida.

Wananchi waliojitokeza katika eneo la tukio

Mwili wa mtoto huyo ambaye anakadiriwa na umri wa siku mbili umekutwa umetupwa katika eneo la kukusanyia taka huku mzazi wa mtoto huyo akiwa bado hajajulikana.

Baadhi ya mashuhuda waliofika katika tukio hilo wameelezea masikitiko yao kwa tukio hilo ambalo amefanyiwa mtoto mchanga asiye na hatia.

Kwa Upande wake Diwani wa kata ya Manyoni mjini bw.Maghembe Machibula na Mwenyekiti wa kitongoji cha Majengo bw. Silvester Msogoti wamewataka wakazi wa kitongoji hicho kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kutoa taarifa za mtu yeyote aliyehusika kumtupa mtoto huyo.

Akithibitisha kupokea mwili wa mtoto huyo, Mganga Mkuu wa Hospitali ya Manyoni, Dokta. Furaha Mwakafwila amesema wamepokea mtoto huyo akiwa ameshafariki ambapo amebainisha kuwa kuwa huenda mtoto huyo amefariki ndani ya masaa 24 mpaka muda waliompokea.