Jumatano , 16th Mei , 2018

Mwenyekiti wa Baraza la vijana Chadema (BAVICHA), Patrick Ole Sosopi, amesema amewahi kushawishiwa na wanachama wa Chama cha Mapinduzi (CCM) ili aweze kuhamia chama hicho tawala.

Ole Sosopi amesema hayo leo Mei 16 akiwa studio za EATV katika kipindi cha KIKAANGONI kinachorushwa kila siku ya Jumatano kuanzia saa 8:00 mchana hadi saa 10:00 za jioni na kuongeza kuwa yeye hana thamani ambayo itaweza kumnunua kwakuwa ni tegemeo la vijana wa CHADEMA nchi nzima.

“Ndiyo nimewahi kushawishiwa na kiukweli ukiwa bora watataka kukuonesha kwamba utakua bora zaidi, kumbe sio sahihi, ubora wa Ole Sosopi unaoonekana leo CHADEMA, kama ningekuwepo CCM inawezekana ninsingepata hata ubalozi wa nyumba kumi, naamini kule hawathamini uwezo bali ni nani anakujua na historia yako” amesema Ole Sosopi.

Kiongozi huyo wa BAVICHA Taifa ameongeza kuwa watu hao walikua wakimshawishi kwa kutumia njia ya kiurafiki kwa kumwambia kuwa kutokana na ubora wake alistahili awepo upande wa Chama cha Mapinduzi (CCM).

Novemba 21, 2017 aliyekuwa mwenyekiti wa Baraza la Vijana Chadema (BAVICHA) Patrobasi Katambi alitangaza kuhamia Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa madai ya kufurahishwa na utendaji kazi wa mwenyekiti wa chama hicho Rais Dkt. John Magufuli