Jumatatu , 13th Nov , 2017

Waziri wa Mali Asili na Utalii Dkt. Hamisi Kigwangalla amelitaka jeshi la Polisi na TAKUKURU kumchunguza aliyekuwa waziri wa wizara hiyo Lazaro Nyalandu, kwa kutumia madaraka yake vibaya wakati wa uongozi wake.

Kigwangalla ametoa kauli hiyo leo alipokuwa akichangia hoja ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa 2017/2018  Bungeni mjini Dodoma, na kusema kwamba wakati wa uongozi wake Lazaro Nyalandu aliikosesha serikali mapato ya bilioni 32 kwa kutosaini sheria ya tozo kwa hoteli za kitalii.

Mbali na tuhuma hizo, Waziri Kigwangalla pia amesema Lazaro Nyalandu akiwa Waziri alitumia helkopta ya mwekezaji mmoja raia wa kigeni kwenye kampeni zake mwaka 2015 wakati kampuni hiyo ilikuwa ikituhumiwa kwa ujangili.

Taarifa hiyo imekuja kipindi ambacho Lazaro Nyalandu amejiondoa CCM na kujiunga CHADEMA, na alishatoa taarifa kwenye mitandao ya kijamii kuwa yataibuliwa mengi baada ya yeye kutoka CCM, na kuwataka watu wayapuuzie kwani hayana ukweli wowote.