Alhamisi , 4th Jun , 2020

Meya wa Ubungo Boniface Jacob amesema kuwa, huenda siku mbili zijazo aliyewahi kuwa Mbunge wa Singida Mashariki Tundu Lissu, ataweza kuzungumza na kueleza yuko wapi na anafanya nini.

Meya wa Ubungo Boniface Jacob, na kulia ni aliyewahi kuwa Mbunge wa Singida Mashariki Tundu Lissu.

Meya Jacob ameyabainisha hayo leo Juni 4, 2020, wakati akizungumza na EATV&EA Radio Digital, kufuatia picha aliyoiweka kwenye ukurasa wake wa Twitter siku za hivi karibuni, akiwa amepiga picha na Tundu Lissu na kuandika maneno ya karibu nyumbani.

"Ile picha ni ya siku za hivi karibuni, na mimi nilifanya vile kama kumkaribisha tu arejee nyumbani, lakini kusema yeye yuko wapi na anafanya nini, atazungumza yeye mwenyewe siku mbili zijazo hata usiwe na papara" amesema Meya Jacob.

Tundu Lissu alikuwa nchini Ubelgiji kwa ajili ya matibabu, baada ya kupigwa risasi na watu wasiojulikana Septemba 2017, karibu na makazi yake Jijini Dodoma, na alipelekwa nchini Kenya kwa ajili ya matibabu na hatimaye alisafirishwa hadi nchini Ubelgiji kwa ajili ya matibabu zaidi.