Alhamisi , 18th Oct , 2018

Siku moja baada ya kuripotiwa kwa tukio la kufa kwa wanafunzi wa watatu katika shule ya msingi ya Emaco iliyopo Mkoani Geita, Jeshi la Polisi mkoani humo limesema tukio hilo halikuwa na uhusiano wowote na imani za kishirikina bali ni kutokana na majanga ya asili.

Pichani mfano wa radi.

Akizungumza na www.eatv.tv Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoani humo, Daniel Shila amesema jeshi hilo lilikamilisha uchunguzi wa tukio hilo ndani ya saa 24 na kufanikiwa kuikabidhi miili ya marehemu kwa ndugu zao kwaajili ya mazishi.

“Tumefanya uchunguzi wa watoto 6 ndani ya siku moja, ni tukio la janga la asili sio kwamba limetokana na mtu. Hakuna mtu anayetengeneza radi, mambo ya kitaalamu yameshafanyika na jana hiyohiyo tumeishakabidhi kwa ndugu kwa ajili ya mazishi.”amesema Daniel  Shila.

Awali, Mkurugenzi wa Shule hiyo, Cosmas Kibela alizungumzia juu ya tukio hilo kuhusishwa na imani za kishirikina kwa baadhi ya wakazi wa maeneo hayo ambapo amesema “watu wanaweza kuwa na imani hizo lakini kwa imani yangu siamini kama linahusika na imani za kishirikina, na wala sitaki kujiingiza zaidi kwenye mitazamo ya watu.”

Miezi miwili iliyopita shule hiyo iliingia kwenye kashfa juu kuwepo kwa mwanafunzi ambaye alitajwa kutaka kuwadhuru  wanafunzi wenzake kupitia sumu, kashfa ambayo ili kanushwa vikali na Mkurugenzi huyo.