Jumapili , 14th Oct , 2018

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt John Pombe Magufuli amesema kuwa mwezi wa kumi na mbili mwaka huu anatarajia kuhamia rasmi makao makuu ya nchi Dodoma kama ilivyokuwa matamanio ya Hayati Mwalimu Julius Nyerere.

Rais, Dkt John Magufuli

Rais Magufuli ametoa kauli hiyo jijini Dar es salaam wakati alipokwenda kumtembelea Mjane wa Baba wa Taifa, Mama Maria Nyerere ambapo kabla ya kufika kwake alitumia fursa hiyo kushiriki nae ibada kanisa la Mtakatifu Petro Oysterbay.

Rais Magufuli amesema “azimio la Arusha ukilisoma unajua kila kitu kuhusu nchi yetu, baba wa taifa mwaka 1973 alisema tuhamie Dodoma ndio makao makuu ya nchi, Dodoma tunahamia na mimi ndio nakaribia kumalizia, mwezi wa 12 nihamie huko.”

“Niwaombe watanzania wenzetu tuendelee kuitunza amani yetu, maana hatuna baba mwingine wakutusimamia zaidi ya baba wa mbinguni, lakini kifo cha baba wa taifa kitufunze watanzania tuwe na mshikamano, na kila mmoja tuendelee kumuombea huko aliko aendelee  kupumzika kwa amani, ameongeza Rais Magufuli.

Kitaifa kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere inafanyika Mkoani Tanga, ambapo mamia ya wananchi wamejitokeza na kushuhudia sherehe hizo ambazo Mgeni rasmi ni Rais wa Zanzibar, Dkt Ally Mohamed Shein.

Oktoba 14 ndio tarehe ambayo Watanzania tunaadhimisha kifo cha Muasisi wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere ambacho kilitokea mwaka 1999 baada ya kuugua kwa muda nchini Uingereza.