Jumapili , 17th Mei , 2020

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt John Pombe Magufuli, amesema kuwa mwanaye wa kuzaa alipata maambukizi ya Virusi vya Corona lakini alijitibu kwa kujifukiza na kutumia maji ya limao na Tangawizi.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt John Pombe Magufuli.

Rais Magufuli ameyabainisha hayo leo Mei 17, 2020, wakati akituma salamu zake kwa Watanzania, ikiwa ni sehemu yake ya ibada katika Kanisa la KKKT Mjini Chato, na kusema kuwa ameamua kueleza hilo ili Watanzania na wao wajue kama naye lilimfika.

"Mimi ninapozungumza hapa nina mtoto wangu alipata Corona, wa kuzaa mimi, alijifungia kwenye chumba, akaanza kujifukizuia, akanywa malimao na Tangawizi, amepona yuko mzima sasa anapiga 'pushup', huo ndiyo ukweli siwezi kusema uongo kwenye madhabahu hapa, wanaweza kufikiri labda mimi halijanipata" amesema Rais Magufuli.

Aidha Rais Magufuli ameendelea kusisitiza kuwa, Tanzania hii hakutokuwa na lockdown na badala yake wananchi waendelee kuchapa kazi zao bila kusahau kuchukua tahadhari.