Jumamosi , 19th Sep , 2020

Rais wa Burundi Evariste Ndayishimiye amempongea Rais Magufuli kwa utendaji kazi wake kwa kuwa ameibadilisha Tanzania kwa kiasi kikubwa, na kwamba anao uhakika kama wananchi watamchagua tena na atapata ushindi wa kishindo katika uchaguzi mkuu ujao.

Kushoto ni Rais wa Burundi Evariste Ndayishimiye na kulia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli.

Rais Ndayishimiye ametoa kauli hiyo hii leo Septemba 19, 2020, wakati akizungumza na wananchi wa Kigoma ikiwa ni ziara yake ya kwanza nchini tangu alipoapishwa rasmi kuwa Rais wa Burundi na kueleza kuwa warundi wengi wanatamani kumpigia kura Magufuli

"Umebadilisha nchi ya Tanzania na Kigoma na mimi hadi nimeshangaa nakupongeza sana, nakupa pole najua uchovu wa kampeni, lakini najua ninao uhakika kwamba wewe kuwa na wananchi wa Tanzania ni kama Baba na watoto, nina uhakika kwamba utashinda uchaguzi, na warundi wote wanasema, ningekuwepo ningechagua Dkt Magufuli", amesema Rais Ndayishimiye.

Mbali na hayo Rais Ndayishimiye akazungumzia masuala ya usalama nchini humo kwa sasa, "Burundi sasa hivi hali ya usalama ni shwari, siyo kama zamani warundi wote tumekaa pamoja na kuzungumza na tukagundua kwamba Burundi hatuna kabila la Kihutu na Kitusi, tukagundua wazungu walitugawa tu, ndiyo sababu tumekwishajiunga hatutarudi tena kwenye machafuko ya zamani".