Jumamosi , 17th Aug , 2019

Mkuu wa Mkoa wa Lindi,Godfrey Zambi amezuia watumishi wa Serikali kwenda likizo kwa muda wa miezi mitatu, ili kusimamia miradi ya Maendeleo na vitambulisho vya wajasiriamali kwenye maeneo yao, na maandalizi ya mapokezi na uzimaji wa Mwenge wa Uhuru.

Zambi ameweka zuio hilo alipokuwa anazungumza katika kikao kazi na watumishi mbalimbali, wakiwemo Ma Ofisa Tarafa na watendaji Kata wa Halmashauri za Wilaya na Manispaa ya Lindi kilichofanyika uwanja wa Ilulu mjini hapa.

Amesema amechukuwa uwamuzi huo kufuatia Shughuli nyingi inazoukabiri Mkoa mwaka huu, kama vile uzimaji mwenge wa Uhuru utakaoitimisha mbio zake na kumbukizi kifo cha hayati Baba wa Taifa, Julius K.Nyerere Oktoba 14 mwaka huu na haraiki ya vijana.

Zambi alisema kutokana na majukumu hayo, amelazimika kuzuia watumishi wote wa Serikali, Wakiwemo Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri za Wilaya na Manispaa, Ma-Ofisa Tarafa, watendaji Kata, vijiji, Mitaa na vitongoji kutoenda likizo, kwa muda hadi pale zitakapokamilika.

Amesema amelazimika kuzuia likizo kwa watumishi kutokana na sababu nne,ikiwemo ujio wa Mwenge wa Uhuru, kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo,Shughuli za vijana na ukamilishaji wa zoezi la uuzwaji wa vitambulisho vya wajasiliamali.

"Kuanzia Leo nazuia likizo zote za watumishi wote wa Serikali hadi mwezi Disemba mwaka huu"Alisema Zambi.

Mkuu huyo wa Mkoa amesema Mkoa una miradi mingi,kama vile ujenzi wa vituo vya Afya, Zahanati na Shule lakini kutokana na kukosa usimamizi wa karibu imekuwa ikilegalega utekelezaji wake.