Jumanne , 18th Feb , 2020

Mbunge wa Arusha Mjini Godbless Lema, amemuomba Waziri wa Mambo ya Ndani George Simbachawene, kuingilia kati suala la kuwakamata wale waliosambaza video zinazoonesha ubovu wa miundombinu ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa kuwa hawana hatia yoyote.

Mbunge wa Arusha Mjini Godbless Lema.

Lema ameyabainisha hayo leo Februari 18, 2020, wakati akizungumza na EATV&EA Radio Digital na kusema kuwa kitendo cha RPC Arusha kumpa onyo kwamba asiingilie suala hilo, kimemshangaza na yeye hatoacha kumuingilia hususani kipindi hiki cha uchaguzi.

"RPC hanipangii, mimi majukumu yangu yameainishwa kwenye katiba ndio maana mimi nampangia hata mshahara wake, kwahiyo nitaendelea kumpangia na kumuingilia, wajibu wa Mbunge ni kupigania haki za watu wanaoonewa na asichukue hatua yoyote kwa waliosambaza hiyo video najua IGP na Waziri Simbachawene wananisikia, nadhani watakuwa wamempa maelekezo" amesema Mbunge Lema.

Jana Februari 17, 2020, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Jonathana Shana, alimpa onyo Lema, kutoingilia kazi za jeshi na kwamba lazima atatekeleza agizo la Mkuu wa Mkoa huo la kuwasaka na kuwakamata wale wote waliohusika kusambaza video hizo, kwani hawakuwa na nia njema na uchumi wa nchi.