Jumamosi , 13th Oct , 2018

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe, amesema serikali haitaendelea kuvumilia kuona watu wanakufa kutokana na ajali zinazotokana na makosa ya kibinadamu ikiwemo ulevi na imekuja na mpango wa kuwapima vilevi madereva.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe.

Akiongea leo jijini Dar es salaam, wakati wa kukabidhi vifaa vya kupima vilevi kwa wasimamizi na waendeshaji wa Treni, TRC na TAZARA,  waziri Kamwelwe amesema madereva watapimwa kiwango cha vilevi ili kujiridhisha kama hawajatumia.

''Kwa kutumia vifaa hivi tutaweza kubaini viwango vya vilevi kwa wafanyakazi hawa, mwanzo wa safari, katikati na mwisho wa safari. Nimatumaini ya serikali kwa kutumia vipimo hivi idadi ya ajali zinazotokana na makosa ya binadamu zitapungua'', amesema Waziri.

Mbali na hilo Waziri Kamwelwe amewataka viongozi wa vyama vya wafanyakazi nchini kutotetea tu wafanyakazi bila kutazama kosa alilofanya.

''Msitetee tu kwasababu ni wanachama wenu, unakuta anakosa au hajafika kazini wewe huchukui hatua ila mwajiri wake akichukua hatua wewe unakuwa wa kwanza kumtetea'', amesongeza.