Jumatano , 18th Apr , 2018

Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano imemtaka mbunge wa Kigoma mjini Zitto Zuberi Kabwe, kuvuta subira juu ya ujenzi wa bandari katika ziwa Tanganyika mkoani Kigoma.

Akijibu swali za Zitto Kabwe lililotaka kujua ni kwa nini serikali haijaidhinisha utangazwaji kwa zabuni za ujenzi wa bandari hiyo mkoani Kigoma licha ya maandalizi kuwa tayari, serikali kupitia Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano John Elias Kwandikwa, amesema ujenzi wa bandari hiyo tayari umeshawekwa kwenye bajeti ijayo. 

“Siyo kweli kwamba serikali imezuia, ujenzi una hatua zake, tunaanza kwenye usanifu, kuweka fedha , kama kuna jitokeza jambo linajitokeza lazima serikali ichukue hatua, nikutoe wasi wasi tusubiri wakati wa bajeti utaona namna tulivyojipanga, maeneo yote ambayo Zitto anataja tumeainisha vizuri kwenye bajeti, ni Jumatatu tutaanza kuwasilisha bajeti ya wizara hii”, amesema Naibu Waziri Kwandikwa.

Kwenye swali lake Zitto Kabwe ameainisha kwamba bajeti ya ujenzi wa bandari hiyo ilishatengwa tangu mwaka 2016/17 na tayari mamlaka ya bandari ilishaweka utaratibu wa manunuzi, na kusema kwamba Wizara imezuia kutangaza zabuni hizo.